Friday, March 2, 2012

Naledi..............


BAADA ya kimya cha muda mrefu, Naledi Fashion House kesho itazindua toleo lake jipya kwa mwaka 2012. Shughuli hiyo itafanyika katika hoteli ya Sea Cliff iliyoko jijini Dar es salaam.
Toleo hilo maalum litakusanya mitindo ya aina nne yenye vionjo vya kiafrika vyenye mahadhi ya zamani. Mitindo hiyo ni pamoja na ile ya kiofisi, ya kawaida, ya mitoko ya jioni na hata ile ya sherehe hususani za harusi.
Mkurugenzi wa Naledi Kemi Kalikawe amesema kuwa lengo hasa la onyesho , pamoja na kuonyesha vipaji vya wabunifu chipukizi ni kuwakumbusha wadau kwamba siku zote ya kale ni dhahabu.
“Na hii ndio sababu kubwa ya shoo hii kuitwa vintage catwalj, kwani tutawaonyesha watu mavazi yanayoendana na mandhari ya kisasa ambayo yana vionjo vya kale. Mavazi hayo yamebuniwa kwa ustadi wa hali ya juu hivyo, hakuna shaka juu ya ubora wake” alisema
Katika onyesho hilo kutakuwepo na vionjo mbalimbali vya kale kama vile utengenezaji wa nywele na mapambo mengine.
Baadhi ya wabunifu chipukizi kutoka nchini watakaoonyesha kazi zao ni pamoja na Mgece Mackory, Annette Charles Ngongi, Bambo Fransis Magingo, Garvas Lushaju , pamoja na Ahmed.Pamoja nao kutakuwepo na wabunifu kutoka nje ya nchi ambao ni Palvika kutoka nchini Uingereza.
Pia kutakuwepo na wabunifu watakaoonyesha mapambo kama vile hereni, mikufu na bangili kwa upande wa Tanzania kutakuwako na Mwandale pamoja na Phoeniz Africa. Na pia kutakuwako na Riri kutoka nchini Kenya.
Mbali na mavazi Kemi amebainisha kuwa wanamitindo wote watakaopambwa jukwaani, watapambwa kwa kutumia sanaa ya zamani na hivyo kuzidi kunogesha zaidi shoo hiyo.
Naledi ni miongoni mwa kampuni za kitanzania zinazobuni mavazi kwa kutumia kanga na vitenge, ikiwa na lengo la kuendeleza utamaduni wa mtanzania na mwafrika kwa ujumla.

No comments:

Post a Comment